IQNA

Sura za Qur'ani Tukufu / 41

Surah Fussilat: Qur'ani Tukufu haiwezi kupotoshwa au kubadilishwa

16:15 - November 19, 2022
Habari ID: 3476113
TEHRAN (IQNA) – Moja ya imani ambayo Waislamu wanashikilia ni kutoweza kupotoshwa kwa Qur'ani Tukufu. Kwa mujibu wa imani hii, Qur'ani Tukufu sasa ni sawa na ilivyokuwa wakati ilipoteremshwa kwa Mtukufu Mtume Muhammad (SAW) na hakuna neno lililoongezwa au kutolewa ndani yake

Huu unachukuliwa kuwa muujiza wa Qur'ani Tukufu pia. Suala hili limejadiliwa katika Surah Fussilat.

Surah Fussilat ni sura ya 41 ya Qur'ani Tukufu, ina aya 54 na iko katika Juzu za 24 na 25 za Qur'ani Tukufu. Ni miongoni mwa Sura za Makki na Sura ya 61 iliyoteremshwa kwa Mtukufu Mtume Muhammad (SAW).

Neno Fussilat maana yake ni "limefafanuliwa kwa undani". Wengine wamelifafanua kuwa na sehemu kadhaa. Neno hilo limekuja katika Aya ya tatu ya Sura na hilo limeipa sura hiyo jina lake.

Sura hii zaidi inahusu kukanusha kwa makafiri Qur'ani Tukufu. Suala hili limetajwa katika sehemu mbalimbali za sura, zikiwemo Aya za kwanza.

Katika Aya ya 26, imetajwa tena: “Na walio kufuru walisema: Msiisikilize Qur'ani hii, na timueni zogo, huenda mkashinda."

Pia katika Aya ya 40, Mwenyezi Mungu anasema: “ Hakika wale wanao upotoa ukweli uliomo katika Ishara zetu hawatufichikii Sisi. Je! Atakaye tupwa Motoni ni bora au atakaye kuja kwa amani Siku ya Kiyama? Tendeni mpendavyo, kwa hakika Yeye anayaona mnayo yatenda.”

Katika aya za mwisho, pia kuna mazungumzo juu ya asili ya Mwenyezi Mungu: “Sema: Mnaonaje! Ikiwa haya yanatoka kwa Mwenyezi Mungu, nanyi ikawa ndio mmeyakataa, ni nani aliye potea zaidi kuliko aliye katika upinzani wa mbali?’” ( Aya ya 52 )

Ukweli kwamba Quran Tukufu haibadiliki ni imani iliyozoeleka miongoni mwa Waislamu ambao kwa kauli moja wanaamini  kuwa Qur'ani wanayoisoma leo ni sawa kabisa na ile iliyoteremshwa kwa Mtume Muhammad (SAW) na hakuna hata neno moja lililoongezwa ndani yake au kuachwa ndani yake. Wafasiri wa Qur'anI Tukufu  na wanazuoni wa Kiislamu wametaja aya na Hadithi mbalimbali kukataa uwezekano wa kupotoshwa kwa Quran. Zinajumuisha aya za 41 na 42 za Surah Fussilat zisemazo:

Hautakifikia upotovu mbele yake wala nyuma yake. Kimeteremshwa na Mwenye hikima, Msifiwa.  Huambiwi ila yale yale waliyo ambiwa Mitume wa kabla yako. Hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka ni Mwenye maghfira, na ni Mwenye adhabu chungu. 

Ili kukiacha Kitabu cha Mwenyezi Mungu, makafiri walipaswa kukanusha kanuni na itikadi tatu zinazounda msingi wa wito wa Uislamu, yaani upweke wa Mwenyezi Mungu, utume wa Muhammad (SAW) na kuamini Siku ya Kiyama. Ndiyo maana Surah Fussilat inaeleza kuhusu kanuni hizi kwa undani na inatoa onyo na habari njema.

Masuala mengine yaliyozungumziwa ndani ya Sura ni pamoja na masharti ya Siku ya Kiyama, sifa za Qur'an na kuteremshwa kwake, viungo vya mwili kama macho, masikio, ngozi n.k, kushuhudia madhalimu, na pia hadithi za watu wa A'di na Thamud.

 

Habari zinazohusiana
captcha