Katika ripoti yao kuhusu wafadhili wa kundi la ISIS, Wabunge wa Kamati ya Masuala ya Kigeni ya Bunge la Uingereza wamesema kundi hilo la kigaidi limekuwa likipewa misaada na kufadhiliwa na familia tajiri katika nchi kadhaa za Kiarabu.
Ripoti hiyo imeongeza kuwa: Hata hivyo ufadhili wa Saudia na washirika wake kwa kundi la kigaidi la ISIS umepungua kutokana na kushuka kwa bei ya mafuta ya petroli na vilevile mashambulizi ya anga yanayolenga vyanzo vya fedha vya kundi hilo na kwamba sasa wapiganaji wa Daesh wanategemea wizi wa kutumia silaha kwa ajili ya kufadhili shughuli zake.
Ripoti ya Kamati ya Bunge la Uingereza pia imeitaka serikali ya Riyadh kutekeleza sheria ya kuwazuia raia wa nchi hiyo kulifadhili kundi la kigaidi la ISIS.
Saudi Arabia ni miongoni mwa wafadhili wakubwa wa kundi la kigaidi la Daesh ambalo linatumia aidiolojia za kitakfiri na itikadi za mamufti wa Saudia.
Waraka wa serikali ya Marekani uliofichuliwa na mtandao wa WikiLeaks
unaonesha kuwa, Wasaudi Arabia ndio chanzo kikubwa cha fedha na misaada
inayotumwa kwa makundi ya kigaidi katika maeneo mbalimbali duniani.