Kwa mujibu wa Televisheni ya Al Mayadeen, Ayman Safadi Waziri wa Mambo ya Nje wa Jordan amesisitiza kuwa, Msikiti wa Al Aqsa ni eneo maalumu la ibada kwa ajili ya Waislamu tu na hivyo utawala wa Kizayuni wa Israel hauna mamlaka katika eneo hilo.
Aidha amesema Msikiti wa Al Aqsa uko katika Quds inayokaliwa kwa mabavu na Israel lakini pamoja na hayo Jordan haitakubali Israel iingilie masuala ya msikiti huo.
Aidha Safadi amesisitiza kuwa, Idara ya Wakfu wa Kiislamu katika Mji wa Quds, ambayo inafungamana na Wizara ya Wakfu ya Jordan, ni taasisi pekee ambayo ina jukumu la kusimamia Msikiti wa Al Aqsa.
Kwa mujibu wa mapatano ya amani baina ya Jordan na utawala wa Kizayuni wa Israel, kuanzia mwaka 1994 msikiti wa al Aqsa uliwekwa chini ya Idara ya Wakfu wa Kiisalmu na eneo hilo limetengwa kwa ajili ya Waislamu pekee kufanya ibada.
Utawala wa Kizayuni unatekeleza misingi mitatu mikuu ambayo ni kuugawa utumiaji wa Msikiti wa Al Aqsa kisehemu na kiwakati, kuchimba mashimo ya chini kwa chini na kandokando ya msikiti na kuyahudisha maeneo ya jirani na mahala hapo patakatifu.
Hii ni katika hali ambayo, Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) limethibitisha tena kwamba msikiti mtukufu wa Al-Aqsa, kibla cha kwanza cha Waislamu ni milki ya Wapalestina.