Uhuru wa kujieleza haumaanishi kuutukana Uislamu, Christoph Schonbrunn aliambia jariida la Asharq Al-Awsat. Alibainisha kuwa kumtusi Mtume Muhammad (SAW) kupitia vikaragosi na kuchomwa kwa nakala ya Qur'ani Tukufu ni vitendo vinavyokiuka uhuru wa kujieleza, huku akikosoa vitendo vya hivi karibuni vya baadhi ya watu ambao wamevunjia heshima Uislamu.
Alionyesha imani yake kwamba uhuru wa kibinafsi unamaanisha kuheshimu wengine na sio kumuudhi kwa njia yoyote.
Aliyasema hayo katika safari yake ya mjini Riyadh, Saudia akiwa ameitikia mwaliko wa Muhammad Al-Issa, Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Waislamu Ulimwenguni.
Matamshi hayo yanajiri wiki kadhaa baada ya wimbi jipya la kuvunjiwa heshima Qur'ani katika baadhi ya nchi za Ulaya.
Rasmus Paludan, mwanasiasa mwenye msimamo mkali wa Denmark na Uswidi na kiongozi wa chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha Stram Kurs (Msimamo Mkali), alichoma nakala ya Quran nje ya Ubalozi wa Uturuki mjini Stockholm mnamo Januari 21 akiwa analindwa na polisi na kwa ruhusa kutoka kwa mamlaka ya Uswidi. .
Wiki iliyofuata, alichoma nakala ya kitabu kitakatifu cha Uislamu mbele ya msikiti mmoja nchini Denmark na kusema kuwa atarudia kitendo hicho kila Ijumaa hadi Sweden ijumuishwe katika NATO.
Wakati huo huo, mwanasiasa wa siasa kali za mrengo wa kulia wa Uholanzi Edwin Wagensveld, kiongozi wa Wazungu Wazalendo wa Kupinga Uislamu (PEGIDA), aliichana nakala ya Qur’ani Tukufu kabla ya kuichoma moto katika maandamano ya kupinga Uislamu huko Enschede, Uholanzi mwishoni mwa Januari.
Vitendo hivyo vililaaniwa vikali na mataifa ya Kiislamu duniani kote ambayo yalitaka serikali za Ulaya kuzuia mara moja matusi kama hayo.
4125651